Millionaire  Ads

Isome hapa Taarifa nzima ya TFF dhidi ya tuhuma za ufisadi zinazoenezwa na gazeti la Nipashe


TFF imejibu hoja zote zilizoandikwa na gazeti la Nipashe la May 8 2017 juu ya tuhuma mbalimbali, kwa mujibu ya Saiti ya TFF tunakuletea yalioandikwa kwenye saiti hiyo.
Gazeti la Nipashe limekuwa likichapisha makala maalum katika matoleo yake ya kuanzia tarehe 8 Mei 2017 yakituhumu Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kujihusisha na ‘ufisadi wa kutisha’.

Gazeti hili limekuwa likitumia maulizo ya kiukaguzi (audit queries) yaliyoibuliwa na wakaguzi wa fedha wa TAC miaka mitatu iliyopita, ambayo hata hivyo tayari yalikwishapatiwa majibu, na kuandika vichwa vya habari vinavyolituhumu shirikisho kujihusisha na ‘ufisadi wa kutisha’. Baadhi ya querry hizi zinahusiana na malipo/marejesho ya miaka ya 2002/03 enzi za FAT.

Wakaguzi wa mahesabu baada ya kufanya kazi yao waliandaa management report ambayo iliibua queries au maswali kuhusu matumizi mbalimbali ya fedha. TFF ilijibu maulizo (queries) hayo kwa ufasaha na taarifa kufikishwa mbele ya mkutano mkuu ambao ulipokea na kukubali majibu hayo.

Hata hivyo gazeti la Nipashe limekuwa likitoa taarifa ya upande mmoja tu ambayo ni ya kupotosha, haina ukweli na inakiuka misingi mitatu ya uandishi wa habari ambayo ni usahihi wa habari (accuracy), kusikiliza pande zote (balance) na kutenda haki na kutoa uzito sawa kwa pande zinazohusika kwenye habari (fairness).

TFF imekuwa ikitafakari dhumuni hasa la chombo hiki kikubwa cha habari kuamua kukiuka misingi hii na kuanza kuporomosha tuhuma nzito kwa viongozi wa TFF bila kuwapa nafasi ya kusikilizwa au hata kuomba majibu yatokanayo na audit queries za wakaguzi wa TAC.

Mwenendo huu wa gazeti la Nipashe wa kukiuka maadili kwa makusudi kipindi hiki muhimu katika historia ya soka Tanzania, unalenga kudhoofisha juhudi za TFF na serikali za kuwahamasisha wananchi kuichangia timu yao ya vijana inayoshiriki mashindano ya mataifa ya Afrika kule Gabon, na pia unalenga kushawishi uchaguzi mkuu wa shirikisho utakaofanyika miezi mitatu ijayo.

Hata hivyo, shirikisho limeona inafaa kutoa ufafanuzi kwa kifupi wa masuala yaliyopotoshwa kwenye magazeti ya Nipashe kwa faida ya wasomaji na wapenzi wa mpira wa miguuu kwa ujumla:-

1.   Mamilioni ya Coca-Cola:

 Baada ya kupokea audit queries, marejesho yalifuatiliwa na yalipatikana.

 2.   Madai ya kuwalipa wadai mbalimbali kama Punchline, Atriums, Michael Wambura, n.k.

Ieleweke kuwa TFF ni taasisi endelevu, hivyo uongozi mpya unapoingia madarakani unapokea mali na madeni (assets and liabilities). Na baada ya kuingia madarakani mwezi Novemba, 2013 uongozi ulikumbana na kadhia ya kupokea vitisho vya mali zake kukamatwa kutokana na malimbikizo ya madeni mbalimbali. Kuna kipindi mali na akaunti za TFF zilikamatwa na madalali wa mahakama kwa nia ya kuziuza kufidia madeni tuliyokuta na ikabidi tuzikomboe ili warejeshewe hasa pale ambapo TFF inakuwa haina pesa kabisa na timu za taifa zinakuwa na mahitaji kama usafiri na kulipia kambi. Viongozi wa TFF hawawezi kukubali timu za taifa zisisafiri kisa TFF haina pesa.

Hivyo TFF ilichukua jukumu la kulipa madeni hayo licha ya kuwa na majukumu mengine ya kuendesha timu za taifa na shughuli nyingine za kiutawala na maendeleo ya mpira wa miguu kwa ujumla.

Baada ya kulipa madeni hayo, kulitolewa maelezo ya kina baada ya kupokea audit queries. Lakini pia ieleweke kuwa uendeshaji wa mpira unahusisha mahitaji mengi ya fedha mengine ya dharura na ikitokea hivyo watu hutoa fedha zao mfukoni ili warejeshewe baadaye.

3.   Kuhamia mjini:

Maamuzi ya kuhamia ofisi mpya kwenye jengo ya PPF yalifanyika na kubalikiwa na Kamati ya Utendaji. TFF ina mamlaka chini ya katiba yake kuhamisha ofisi ndani ya mkoa bila kuomba ridhaa ya Kamati ya Utendaji. Kwa hiyo, halikuwa wazo wala maamuzi ya mtu mmoja bali ilikuwa ni pendekezo lililopitishwa na wajumbe wa Kamati ya Utendaji.

TFF ilihamishia ofisi mjini ili kuwa katika mazingira mazuri zaidi ya utendaji na kuboresha mawasiliano. 

Na kuhama huko kwa muda kulifanyika wakati ofisi za TFF zinakarabatiwa. Ilikuwa ni kupisha mradi wa uendelezaji wa Uwanja wa Karume.

PPF ni Shirika la Umma ambalo wakati huo kulingana na ushindani wa kupata ofisi mjini ilionekana kuwa nafasi ya kukidhi mahitaji ya TFF.

Kwa hali ya mahitaji ya “Corporate World” hasa kwa kuangalia dunia ya kisasa za uendeshaji  mpira unaotegemea corporate world kwa vyo vyote ile iko siku TFF itahamia mjini na Ofisi za Uwanja wa Karume kubakia ni Technical Center kama ilivyo kwa nchi kama Zimbabwe, Afrika Kusini, Senegal nakadhalika.

4.   Ukwepaji kodi:

TFF imekuwa ikilipa kodi zake zote na imekuwa ikishirikiana kwa karibu sana na TRA kuhakikishia hakuna malimbikizo. Kuna suala la kodi za kabla ya mwaka 2013 ambalo pamoja na mazungumzo na serikali kuendelea bado TFF imekuwa ikiendelea kulipunguza na mpaka sasa imelipa zaidi ya shilingi bilioni moja ndani ya miaka mitatu.

5.   Mikataba ya manunuzi na ukarabati wa jengo:

Manunuzi ya TFF yanatokea kadiri mahitaji yanavyojitokeza na upatikanaji wa fedha. Na ieleweke kuwa TFF ni taasisi isiyo ya kiserikali na haibanwi na sheria ya manunuzi iliyotungwa na Bunge. Na manunuzi mengine yanafanyika kwa kutumia fedha za FIFA ambazo mrejesho wake unakuwa wa kuridhisha ndio maana mpaka sasa FIFA waniamini TFF.

6.   Kutokuwepo na mkaguzi wa mahesabu wa ndani:

Suala la kuwa na mkaguzi wa ndani ni muhimu katika taasisi yoyote lakini vilevile taasisi inaweza kuwa na muundo ambao una udhibiti sawasawa na ukaguzi wa ndani. Hata hivyo inahitaji maamuzi ya kamati ya utendaji ili kuweza kubadilisha muundo wa shirikisho (Organization Chart). Na siku zote kamati ya utendaji huyafanyia kazi maoni ya wakaguzi na kuyatekeleza kutegemea mahitaji na wakati.

7.   Kutumia interns kufanya kazi:

TFF inaamini katika kuwapa vijana nafasi na hata kuwapa uzoefu wale wanaotoka vyuoni.Kila mwaka TFF hupokea vijana kutoka mashuleni na vyuoni ambao miongoni mwao wamekuja kuwa watumishi wa kuajiriwa baada ya masomo yao. TFF itaendelea kuwapa uzoefu vijana katika kada mbalimbali huku wakisimamiwa na viongozi wazoefu walio ndani ya shirikisho.

8.   Ajira ya Edgar Masoud (RIP):

Upo uthibitisho wa muhtasari wa Kamati ya Utendaji unaoonyesha kuwa utaratibu wa ajira ya aliyekuwa Mkurugenzi wa Fedha, hayati Edgar Masoud na kusitishwa ajira yake ulifuata taratibu zote ikiwa ni pamoja na maamuzi ya kawaida kupitishwa na Kamati ya Utendaji ya TFF.

9.   Mkutano na Waandishi wa Habari:

Kama Rais wa TFF, anaweza kufanya mkutano na wanahabari yaani press conferences nje ya Karume. Nyingi huwa tunafanyia nje ya ofisi kulingana na mahitaji vikiwa vikao vya Kamati ya Utendaji na kamati mbalimbali.

10.Ukarabati:

Ukarabati huu ulifanyika kwa fedha za FIFA, kanuni za FIFA zinasoma hivi matumizi ya chini ya dola 50,000 hayahitaji zabuni/tenda. Isitoshe FIFA walileta pesa ili kazi ifanyike. Kazi hii ilifanyika taratibu na pole pole kwa kiasi TFF iloivyokuwa inapata pesa. Huu utaratibu uko mpaka leo.

11.Tuhuma kuhusu matumizi ya fedha za wafadhili (sponsors):

TFF imekuwa ikivutia wafadhili mbalimbali kuwekeza katika TFF. TFF huwa inaandaa program zake na ratiba kwa kutegemea fedha za ufadhili. Lakini mara nyingi ipokeaji wa fedha za ufadhili umekuwa ukichelewa na kukuta program mbalimbali zilikwiaanza/kumalizika. Ili kutokwamisha program mbalimbali TFF huwa ina utaratibu wa kutumia pesa toka vyanzo mbalimbali ili kukidhi mahitaji ya program na kurudisha pesa hizo wakati wafadhili wakilipa. Vyanzo hivi ni pamoja na kutumia pesa za ruzuku/wafadhili wengine/kuazimwa pesa kwa muda mfupi. Huu utaratibu ni muda mrefu kuanzia miaka ya tisini hadi sasa.

Utaratibu huu umekuwa ukitumiwa kwa sababu shughuli za mpira zinatokea katika mazingira ya dharura na lazima zifanyike. Kama kuna mechi za kucheza za timu ya taifa na mfadhili hajatoa pesa, lazima TFF ikope kutoka vyanzo vingine ikiwemo watu binafsi, kama viongozi wa shirikisho na mashirika ili kuhakikisha taifa halipati adhabu kwa kutoshiriki mashindano husika au kufanya maandalizi yanayotakiwa.
Tunapenda kuviasa vyombo vya habari kufanya kazi yao kwa weledi. Ushabiki au kuandika habari kwa kupotosha kutaathiri mpira wa miguu Tanzania. Kutawakatisha tamaa mashabiki na kuwakimbiza wadhamini. Uchaguzi unapita lakini, mustakabali wa taifa unabaki palepale. Uweledi uwepo katika kuripoti kwa lengo la maendeleo ya mpira wa miguu
Chanzo http://www.tff.or.tz/news/872-taarifa-za-uongo-na-uzushi-zinazochapishwa-na-nipashe


Millionaire  Ads

Share :

Facebook Twitter Google+
0 Comment untuk "Isome hapa Taarifa nzima ya TFF dhidi ya tuhuma za ufisadi zinazoenezwa na gazeti la Nipashe"

Back To Top